Bi Fatma bint Baraka maarufu Bi Kidude akisisitiza kwamba yeye ni mzima hasa kwa wale waliojaribu kumzushia kwamba amefariki ila miguu ndiyo inamsumbua kwa sasa.
Makamu wea Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad akiomba
dua pamoja na msaniii mkongwe wa muziki wa Taarab nchini Bi Fatma bint
Baraka alipomtembelea.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amefanya
ziara ya kuwatembelea wagonjwa na wazee kwa ajili ya kuwapa pole na
kuwafariji katika maeneo mbali mbali ya Zanzibar.
Miongoni mwa wagonjwa waliotembelea na Maalim Seif ni msanii maarufu
hapa Zanzibar, Bi. Fatma binti Baraka maarufu Bi. Kidude ambaye
anasumbuliwa na maradhi ya miguu kwa wiki kadhaa sasa.
Bi. Kidude akizungumza na Maalim Seif huko nyumbani kwa mwanawe
Kihinani, Wilaya ya Magharibi Unguja, alimueleza kuwa anasumbuliwa na
maradhi ya miguu, lakini amekuwa akifanya shughuli zake nyingi za
kawaida.
Hata hivyo, Bi. Kidude alisema amesikitishwa sana na kitendo cha baadhi
ya watu kueneza uvumi kwamba amefariki wakati bado ni mzima na anafanya
shughuli zake kama kawaida.
Alimueleza Maalim Seif kuwa kitendo cha watu hao licha ya kumsikitisha
yeye binafsi, pia kimesababisha usumbufu na hofu kubwa miongoni mwa
jamii na baadhi ya watu ambao walilazimika kufunga safari kuja Zanzibar
kutoka nchi mbali mbali.
“Kuna watu wameeneza taarifa za uongo kwamba nimekufa, wapo watu
waliofunga safari kutoka nchi tafauti kuja Zanzibar, lakini walipofika
walishangaa kuniona nipo hai”, alisema Msanii huyo maarufu wa muziki wa
taarab hapa Zanzibar na Afrika Mashariki.